MSD YATUNUKIWA TUZO KWA KUWEZESHA MATIBABU YA MOYO NCHINI
Bohari ya Dawa (MSD) imetunukiwa tuzo maalum na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kutambua mchango na ushirikiano wake katika kuboresha huduma na matibabu ya Programu za Moyo nchini.
Tuzo hiyo maalum, imekabidhiwa na Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mhe. Dkt. Nassor Ahmed Mazrui, wakati akifunga mkutano wa siku tatu wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo, ulioandaliwa na taasisi hiyo ya JKCI, na kukutanisha Wadau mbalimbali, wakiwemo viongozi, madaktari, watafiti, wasambazaji Dawa na Vifaa tibawa visiwani humo.
MSD imekuwa mshirika muhimu wa JKCI katika kuboresha huduma za programu za Moyo nchini, kwa kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji wa uhakika wa dawa, vifaa tiba, vitendanishi kwa ajili ya uchunguzi na matibabu ya moyo nchini.
Aidha, MSD imehakikisha inasambaza dawa na vifaa tiba vya kisasa kwa JKCI, ikiwemo mashine zenye teknlojia ya Akili Mnemba (AI), hatua ambayo imesaidia kuboresha afya za watanzania wenye changamoto za magonjwa ya moyo.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD) ambao ni moja ya wadhamini wakuu wa mkutano huo alisema, JKCI ni moja ya wateja wakubwa wa bohari hiyo ambao wamekuwa wakishirikiana kwa karibu katika kuhakikisha wananamsaidia Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kuboresha sekta ya afya kwa Watanzania kwa kuwa na huduma bora.
Alisema, taasisi hiyo imekuwa ni wadau wakubwa kwa MSD ambao wanatoa oda ya mahitaji yao kwa wakati na yaliyo na maoteo sahihi na wamekuwa wakihakikisha wanashirikiana kupata wazabuni, kujifunza teknolojia mpya, kununua bidhaa na vifaa vyenye uhitaji.
Naye Meneja wa MSD Kanda ya Dar es Salaam Betia Kaema alisema, lengo la kushiriki mkutano huo ni kutanua wigo kwa wataalamu wa magonjwa ya moyo Afrika kutambua uwezo wa MSD katika kuhudumia sekta hiyo, sambamba kutanua wigo wa ushirikiano na wadau wengine waliohudhuria mkutano huo.
- Log in to post comments