Huduma za Ugomboaji
Kitengo cha Ugomboaji ni kitengo cha kimkakati kinachofanya kazi kwa kujitegemea chini ya kurugenzi ya Manunuzi. Kitengo hiki kimesukwa vizuri kikiwa na maeneo sita (6) ambavyo ni: Vibali vya Uingizaji na Uondoshaji mizigo nchini, Tangazo (declaration), Uhasibu, Bandari, Viwanja vya ndege na Wakala wa meli. Kitengo huandaa malengo, mipango mkakati na vipimio vya ufanisi kwa ajili ya ugomboaji wa haraka.
Bohari ya Dawa (MSD) hugomboa bidhaa za afya ambazo 90% huagizwa kutoka nje ya nchi. Taratibu za manunuzi tajwa hapo juu kutoka nje ya nchi zinakamilika baada ya taratibu za ugomboaji wa shehena kutoka nje ya nchi kupitia bandarini, viwanja vya ndege na mipakani kumfikia mlaji wa mwisho. Hivyo, kitengo hiki ni kiungo kinachounganisha mnyororo wa uingiaji wa shehena kutoka nje ya nchi na mnyororo wa usambazaji wa bidhaa za afya, vitendanishi vya maabara kwenye vituo vya afya na hospitali teule nchini.
Kitengo cha Ugomboaji pia huandaa, kuingiza na kutunza takwimu muhimu za shehena za Afya ambazo ni chanzo cha kanzi data ya shehena zilizoingia na kutoka nchini kwa ajili ya kanzidata ya Taifa, inayosaidia Serikali kukusanya kodi stahiki na takwimu za Taifa kwa dawa na vifaa tiba vilivyoingia na kutoka nchini.
Wateja wa kitengo cha Ugomboaji;
- Wizara ya Afya, UNICEF, PERFAR, NMCP, NACP, Mpango wa Afya wa Uzazi , Mpango wa Chanjo wa Taifa, Mpango wa Taifa wa kupambana na Kifua kikuu na Ukoma (NTLP), Mpango wa Magonjwa yasiyopewa Kipaumbele(NTD),Mpango wa Chakula na Lishe Tanzania.
- Washitiri wote wa Bohari ya Dawa wanaoleta dawa na vifaa tiba kwa utaratibu wa DDP
- Shehena zote zinazonunuliwa na MSD na kuletwa nchini mpaka bandarini kwa utaratibu wa CFR (Cost and Freight Delivery term)
Tozo za ugomboaji
- MSD ni taasisi ya serikali ambayo haitengenezi faida. Kitengo cha MSD cha ugomboaji hutoza kiasi cha chini cha ada ili kurejesha gharama za kawaida za uendeshaji.
- Muundo wa malipo wa MSD hupitiwa kila mara na wadau wakiwemo washirika wa maendeleo na Wizara ya Afya.
- Ada ya ugomboaji inategemea zaidi idadi ya kontena, asili ya bidhaa na njia ya usafirishaji.
- Gharama zingine ni gharama halisi zinazotokana na huduma ya washitiri kwenye myororo wa ugomboaji.
- Bili ya mteja hutayarishwa mara tu baada ya kugombolewa kwa shehena.